Wednesday, July 11, 2012

VIFO vya wapendanao wawili


VIFO vya wapendanao wawili, Yusuph Badi na mchumba wake aliyefahamika kwa jina la Pendo waliofariki dunia Keko Toroli jijini Dar es Salaam kutokana na kuungua kwa moto vimezua utata baada ya mwanaume kukutwa akiwa amekaa kando ya mwanamke ambaye alikutwa akiwa amelala chali chumbani.
Mwandishi wetu aliyefanya uchunguzi wa vifo vya wapendanao hao, aliambiwa na mashuhuda kuwa tukio hilo limezua utata baada ya wawili hao kukutwa katika hali hiyo na hakukuwa na hitilafu ya umeme na marehemu hao hawakuwa na mshumaa wala kibatari chumbani mwao.
Rafiki wa marehemu Pendo, aliyejitambulisha kwa jina la Fatuma alikuwa na haya ya kusema: “ Nilifika nyumbani kwa Pendo jioni ya Julai tano mwaka huu na tukazungumza hadi saa tano usiku nikaondoka. Saa saba nikapata taarifa kuwa nyumba yao imeteketea kwa moto.
“Mazingira waliofia hawa wenzetu yana utata mkubwa, watu wanajiuliza moto huo umetokana na nini kwa kuwa ndani ya chumba chao hakukuwa na mshumaa wala kibatari, walikuwa wakitumia tochi tu,” alisema Fatuma.
Naye mjumbe wa mtaa huo wa Keko Toroli, Zubeda Sobo alisema: “Nilisikia watu wakilia katika nyumba hiyo huku moto ukiwaka. Niliamuru watu wafungulie mota kwa ajili ya kusukuma maji ya kuuzima moto.
“Baadaye tulifanikiwa kuingia ndani na kukuta maiti ya mwanaume ikiwa imeketi kwenye kiti na mwanamke akiwa amelala chali kitandani, ajabu ni kwamba chaga za kitanda, simu na noti ambazo zilikuwa kwenye waleti, hazikuungua.
“Kwa kweli nashindwa kuelewa mazingira ya moto huu na wananchi wengi tumepigwa na butwaa,” alisema kwa masikitiko mjumbe huyo.
Alibainisha kuwa polisi na zima moto walifika moto ukiwa umeshazimwa na wananchi.
Marehemu Yusuph alizikwa katika makaburi ya Chang’ombe na Pendo alisafirishwa Ijumaa wiki iliyopita kwenda Arusha kwa mazishi.

No comments:

Post a Comment