Thursday, November 22, 2012

Shule ya Msingi Ndonga: Mtihani wa Taifa hubebwa kichwani, Haijawahi kukaguliwa tangu mwaka 1995





share
NI safari ya siku mbili  kutoka mjini Songea makao makuu ya mkoa wa Ruvuma hadi kuweza kuifikia shule ya msingi Ndonga iliyopo wilayani Nyasa mwambao mwa ziwa Nyasa.
Basi linaishia katika mji mdogo wa Liuli, Ziwa Nyasa na kutoka hapo inakulazimu kukodi pikipiki hadi katika kijiji cha Njambe kata ya Kihagara ambapo ndiyo mwisho wa usafiri wa pikipiki na kuanzia hapo inakulazimu kutembea kwa miguu kwa takribani saa moja hadi kukifikia kijiji cha Ndonga!
Shule ya msingi Ndonga imejengwa juu ya mlima wa Liwundi, unapofika katika kijiji cha Ndonga inakulazimu kupanda mlima wenye mwinuko mkali wenye makorongo kwa takriban zaidi ya saa moja hadi kufika kileleni ndipo unakutana na shule hii.
Asilimia 90 ya wanafunzi wanaosoma katika shule ya msingi Ndonga wanaishi chini ya mlima hivyo inawalazimu kwa siku tano yaani Jumatatu hadi Ijumaa kupanda  na kushuka mlima kwa saa mbili hali ambayo imesababisha shule hiyo kukabiliwa na utoro uliokithiri wa wanafunzi ambao unafikia kwa siku kati ya asilimia 60 hadi 70.
Wanafunzi wa darasa la tatu katika shule ya msingi Ndonga wilayani Nyasa mkoani Ruvuma wakisomea darasa ambalo halijaezekwa kwa mwaka mmoja sasa mvua na jua vikiwakabili
Akizungumza kwa niaba ya mwalimu mkuu, mtaaluma wa shule ya msingi Ndonga Amos Kilongo anasema shule hiyo inakabiliwa na changamoto nyingi ambazo zinachangia kushusha taaluma kwa wanafunzi mwaka hadi mwaka na kwamba hakuna juhudi zozote zinazofanywa na serikali ya kijiji wala ngazi ya wilaya kuzitafutia ufumbuzi changamoto hizo.
“Nakupongeza sana kwa kuweza kupanda mlima wenye muinuko mkali na kufika hapa shuleni, hatujawahi kupokea wageni kutoka ngazi ya wilaya tangu shule hii ilipoanzishwa mwaka 1995, shule haijawahi kukaguliwa tangu mwaka 1995 ilipokaguliwa wakati inaanzishwa’’, alisisitiza.
Sera ya elimu inaeleza wazi kuwa kila shule ya msingi inatakiwa angalau ikaguliwe kila mwaka kwa lengo la wakaguzi kuwakumbusha walimu na kutoa mwongozo wa ufundishaji wenye tija na uendeshaji wa shule kulingana na maelekezo ya wizara ya elimu.
Robo tatu ya wanafunzi 309 wanaosoma katika shule ya Ndonga hawana viatu hali ambayo inawaathiri kiafya kwa kuwa wanaingia katika vyoo bila kuvaa viatu
Kulingana na mwalimu wa shule ya Ndonga, shule hiyo yenye wanafunzi 309 wanaosoma kuanzia darasa la awali hadi la saba inakabiliwa na upungufu mkubwa wa vyumba vya kusomea hali inayosababisha darasa la awali lenye wanafunzi 37 kusomea chini ya mti.
Anabainisha kuwa shule hiyo ina vyumba vinne tu vya madarasa hali ambayo imesababisha madarasa mawili kusomea katika chumba kimoja na kwamba kuna madarasa mawili ambayo yameezuliwa na upepo kwa zaidi ya mwaka mmoja hayajaezekwa hali ambayo inasababisha wanafunzi kusomea huku wakipigwa na jua na mvua.
“Mazingira duni ya kujifunzia yaliopo katika shule hii yamesababisha utoro wa wanafunzi kufikia kati ya asilimia 60 hadi 70 kwa siku,walimu tunafanyakazi katika mazingira magumu, shule ina nyumba moja tu ya mwalimu mkuu yenye vyumba vitatu ambayo tunaishi   walimu  watatu na familia zetu, mimi nimeamua kuishi jikoni kwa kuwa mwalimu mkuu ana familia kubwa hali ni mbaya’’, alisema kwa uchungu.
Haya ni majengo ya vyumba viwili vya madarasa katika shule ya msingi Ndonga wilayani Nyasa ambavyo viliezuliwa na kubomoka tangu mwaka jana,wanafunzi wamekuwa wanasomea huku wakipigwa na jua
Mwalimu wa taaluma katika shule hiyo Amos Kilongo anasema hali ni mbaya kutokana na mazingira duni yaliyopo katika shule hiyo ambapo takwimu za ufaulu kuanzia mwaka 2007 hadi 2011 zinathibitisha kiwango cha ufaulu kuwa chini ambapo shule hiyo hivi sasa ina wanafunzi 50 wasiojua kusoma, kuandika na kuhesabu.
Mwaka 2011 wanafunzi waliohitimu darasa la saba katika shule hiyo walikuwa ni 29 waliofaulu ni wanafunzi watano (5) kati yao wavulana ni  wanne na msichana mmoja, mwaka 2010 waliohitimu walikuwa ni 24, waliofaulu ni wavulana wawili tu, mwaka 2009 waliohitimu walikuwa wanafunzi 32, waliofaulu ni wanane kati yao wavulana watano na wasichana watatu, mwaka 2008 waliohitimu walikuwa 60 waliofaulu 48 kati yao wavulana 22 na wasichana 26.
Hata hivyo anabainisha kuwa mwaka 2007 katika shule hiyo hapakuwepo na wanafunzi wa darasa la saba kutokana na wanafunzi wachache waliofaulu darasa la nne ambao waliunganishwa na darasa la tatu hivyo kuwa wanafunzi 60 waliohitimu mwaka 2008.
“Kutokana na mazingira duni ya shule hiyo ikiwemo kijiji kukosa barabara ya kuweza kupita gari, kila mwaka wakati wa mitihani ya Taifa ya darasa la saba shule hiyo imepewa masafa (route) maalum ambapo gari la mitihani linaishia katika kijiji cha Njambe na baada ya hapo mkuu wa msafara mlinzi pamoja na msimamzi  wanabeba mitihani kichwani na kutembea kwa zaidi ya kilometa saba hadi juu la mlima ambapo ipo shule hii’’, alisema.
Walimu watano wote wanaume wanaofundisha katika shule hii wakiwemo Gorge Mbapira, Joel Makelele, Amos Kilongo Edward Msuya na Atanas Mhagama wamekata tamaa kuendelea kufundisha katika mazingira duni ambayo yanawakosesha huduma zote muhimu ikiwemo mawasiliano, afya, usafiri, maduka na huduma zote muhimu.
Mratibu elimu kata ya Kihagara Severine Ngwenya anasema shule ya Ndonga licha ya kupewa fedha za mpango wa uboreshaji wa elimu ya msingi MMEM mwaka 2002 hadi 2005 bado mazingira ya shule hiyo ni duni kwa kuwa hakuna chumba hata kimoja cha darasa ambacho kimepigwa sakafu badala yake wanafunzi wanasomea kwenye vumbi.
David Mkali afisa elimu wilaya ya Mbinga ambaye anasimamia wilaya mpya ya Nyasa mkoani Ruvuma
“Hali ya shule ya Ndonga kwa ujumla wake ni mbaya na haifai kwa kufundishia na kujifunzia, shule haifikiki kwa gari wala pikipiki bali kwa mguu unapanda mlima kwa saa mbili, hata wilayani hawajawahi kufika katika shule hiyo’’, alisema.
Edward Ndunguru afisa mtendaji wa kijiji cha Ndonga anaitaja mikakati ambayo inachukuliwa hivi sasa na kijiji hicho ni kufyatua tofali 200,000 hata hivyo tofali zilizofyatuliwa ni 60,000 ambazo zitatumika kwa ajili ya kuongeza vyumba vya madarasa na nyumba za walimu katika shule hiyo.
Mbunge wa jimbo la Mbinga mashariki Kapt. John Komba ambaye shule hiyo ipo katika jimbo lake amekiri kijiji cha Ndonga kuwa ni miongoni mwa vijiji ambavyo vinamsumbua kichwa, hata hivyo amesema yupo tayari kusaidia kutoa vifaa vyote vya ujenzi wa shule hiyo  iwapo wananchi watakubali kuihamisha shule kutoka mlimani na kuijenga eneo  linalofikika kirahisi.
Afisa elimu msingi katika Halmashauri ya wilaya ya Mbinga David Mkali ambaye anawajibika katika wilaya ya Nyasa amesema ameandaa takwimu za mapungufu mbalimbali yaliyojitokeza katika shule za msingi ikiwa ni pamoja na upungufu wa vyumba vya madarasa, madawati, walimu na nyumba za walimu kisha kuweka mpango mkakati wa kukabiliana na matatizo hayo.
“Natambua changamoto zinazoikabili shule ya msingi Ndonga, kijiografia shule hiyo haifikiki hali ambayo inasababisha wakaguzi kushindwa kwenda kuikagua kila mwaka hata wakati wa mitihani inakuwa na route maalum, shule kuihamisha toka mlimani ni gharama kubwa sio jambo rahisi inawezekana ukawa mpango wa muda mrefu’’, alisema Afisa elimu.
Afisa elimu huyo ameitaja mikakati mingine ya kuinua kiwango cha ufaulu kuwa ni kuzitembelea shule za msingi kwa kushirikiana na idara ya ukaguzi wa shule ili kufuatilia utendaji kazi wa walimu na kusikiliza changamoto zinazowakabili na kuzitafutia ufumbuzi wa kudumu.

No comments:

Post a Comment