Tuesday, July 17, 2012

Wanaume nao Kutumia Sindano za Kupangilia Uzazi

 Baada ya wanawake kwa miaka mingi kuwa ndio wenye jukumu la kutumia vidonge na njia nyingine katika kupangilia uzazi, watafiti nchini China wamekamilisha utafiti wao ambao utawasaidia wanaume kuwasaidia wanawake jukumu hilo baada ya kutoa sindano kwaajili ya wanaume zitakazosimamisha uzalishaji wa mbegu za kiume kwa muda Wanasayansi nchini China wamekamilisha utafiti wao wa sindano kwaajili ya wanaume ili kusaidia kuzuia mimba zisizohitajika.
Sindano hizo zinasimamisha kwa muda uzalishaji wa mbegu za kiume na watafiti hao walisema kwamba uzalishaji wa mbegu za kiume unaweza ukaendelezwa muda wowote ule.
Watafiti hao waliwatoa wasiwasi wanaume kwa kusema kuwa hakuna madhara yoyote yanayotokana na matumizi ya sindano hizo.

Kwa miaka mingi wanawake wamekuwa wakitumia vidonge na njia nyingine mbali mbali za kuzuia mimba zisizohitajika huku wanaume wakibakia na chaguo moja tu ambalo ni matumizi ya kondomu au kufunga kizazi kabisa kwa njia ya vasektomi.


Wanaume 1,000 wa nchini China wenye umri kati ya miaka 20 na 45 ambao kila mmoja wao alikuwa tayari ana mtoto mmoja au zaidi walishirikishwa kwenye majaribio ya sindano hizo kwa kuchomwa sindano hizo kila mwezi kwa muda wa miezi 30 mfululizo.


Majaribio hayo yalionyesha mafanikio makubwa kwani katika watu 1,000 ni mtu mmoja tu ndiye aliyefanikiwa kumpa ujauzito mpenzi wake wakati akiendelea na sindano hizo.


Mwisho wa utafiti huo, mfumo za uzazi wa wanaume wote walioshiriki kwenye utafiti huo ulirudi katika hali yake ya kawaida isipokuwa wanaume wawili tu.Wanasayansi wamesema watautumia utaalamu uliotumika kujaribu kutengeneza vidonge vitakavyotumiwa na wanaume kusaidia kuzuia mimba zisizohitajika.


Hata hivyo wanasayansi hao walikumbusha kwamba matumizi ya sindano hizo hayamaanishi kwamba ndiyo yatakuwa kinga ya magonjwa ya zinaa.


"Tunawahimiza watu watumie kondomu ili kujikinga na magonjwa ya zinaa" walisema watafiti hao.

No comments:

Post a Comment